Wakulima Kupata Mkopo wa vifaa kuelekea Maadhimisho ya Nanenane
Katika jitihada za kuhakikisha wakulima wanapata nafuu na kilimo
kinapiga hatua, kampuni ya EFTA kwa kushirikiana na GF Truck
zimetangaza kampeni mpya ya kukopesha wakulima vifaa vya kilimo, ikiwa
ni pamoja na magari ya kubeba na kusafirisha mazao, kuelekea kilele
cha maadhimisho ya Sikukuu ya Nanenane.
Akizungumza leo, Julai 26, 2024, jijini Dar es Salaam, Mkuu wa Mauzo
na Masoko wa EFTA, Clerious Asiel, amesema kuwa wameamua kuingia
katika makubaliano hayo ili kusaidia wakulima kwani kilimo chenye tija
kinahitaji matumizi ya vifaa vya kisasa.
"Kwa kampeni hii, tunalenga kuhakikisha kuwa wakulima wanakopeshwa
vifaa vya kilimo ili waweze kufanya kilimo chenye tija na manufaa kwa
haraka. Wakulima wengi hawana fedha ya kulipa papo hapo ila wanamiliki
mali ambazo ziko shambani, hivyo kupitia mpango huu wa GF Truck,
tutaweza kumpatia mkulima kifaa chochote anachohitaji kupitia EFTA,"
alisema Asiel.
Mkurugenzi wa Masoko na Mauzo wa GF Truck, Salman Karmal, aliongeza
kuwa lengo lao ni kusaidia wakulima wa Tanzania kujikwamua kupitia
kilimo.
"Hivyo, mtu yeyote atakayeweza kununua kifaa kutoka kampuni ya GF
Truck atanufaika na kampeni hii, hususan katika msimu wa Nanenane
unaozinduliwa kuanzia Agosti 1, huku maadhimisho ya kitaifa
yakifanyika mkoani Dodoma," alisema Karmal.
Kampeni hii inatarajiwa kuwasaidia wakulima wengi nchini kwa
kuwawezesha kupata vifaa vya kisasa vitakavyorahisisha shughuli zao za
kilimo na kuongeza uzalishaji.
Mwisho
Негізгі бет Maadhimisho ya Nanenane kuleta neema kwa Wakulima kwa Kupata mkopo wa vifaa
Пікірлер