ALIYEKUWA Mkuu wa Mkoa wa Singida,Peter Serukamba amewaaga watumishi na wananchi wa mkoa huu na kusema anaondoka katika mkoa huo huku akiwa ameacha alama Singida kutokana na kuhamasisha matumizi ya mbolea kutoka tani 2200 zilizokuwa zikitumika mwaka 2022 hadi kufikia tani 7,000.
Serukamba ambaye amehamishiwa katika Mkoa wa Iringa, alitumia nafasi ya kuwaaga watumishi na wananchi kwenye kikao cha Kamati ya Ushauri ya Mkoa (RCC) kilichofanyika jana.
Alisema wakati anateuliwa kuwa Mkuu wa Mkoa wa Singida 2022 alikuta wananchi hawaamini katika kutumia mbolea lakini baada ya kuhamasisha mwaka jana zimeletwa tani 7000 za mbolea.
Alisema mipango aliyokuwa amejiwekea ni kuendelea kuwahamasisha wananchi kutumia zaidi mbolea yake hadi kufikia tani 15,000 kwani matumizi ya mbolea yakiongezeka uzalishaji wa mazao utakuwa mkubwa na hivyo wananchi kuondokana na umaskini.
Serukamba alisema alipoletwa Singida alijiwekea malengo ya kufanya kazi kwa bidii ili watu kama ni suala la kumsema wamseme kwa mambo mengine na sio la kufanya kazi kwa ajili ya kuwaletea maendeleo wananchi wa Mkoa wa Singida.
"Wakati nimekuja Singida nilikuta tatizo kubwa lilikuwa ni kutikamilika kwa wakati miradi ya maendeleo lakini hivi sasa inaisha kwa wakati,mnaobaki muendeleze hilo kusimamia kwa karibu miradi na msipofanya hivyo halafu mkarudi kama ilivyokuwa huko nyuma mtanifanye nionekane mimi nilikuwa pengine ni shujaa," alisema.
Alisema kuwepo kwake Singida ilikuwa ni mipango ya Mungu hivyo kama wapo watu ambao pengine watasherehekea kuondoka kwake itakuwa ni ujinga tu kwani kila mtu ana safari yake kimaisha.
"Mimi nina safari kwa hiyo ukishangilia kuondoka kwangu utakuwa ni ujinga tu,sikuwahi kufikiria kwenda Iringa,namshukru Rais Samia Suluhu Hassan ambaye ndiye ameamua kunipeleka Iringa na anazo sababu zake," alisema.
Alisema kwa Mkoa wa Singida yeye (Serukamba) alikuwa RC wa 22 ambapo katika orodha wapo waliokaa muda mfupi sana katika utumishi lakini angalau yeye amekaa mwaka mmoja na miezi saba kuwatumikia wananchi wa Mkoa wa Singida.
Aidha, aliwashukru watendaji kwa ushiriano waliokuwa wanampa na kwamba inawezekana baadhi wanaweza walikuwa hawafurahii na staili yake ya uongozi lakinj yote alikuwa anayafanya kwa ajili ya kuwaletea maendeleo wananchi.
"Hakuna mtu aliyepanga mimi niwepo hapa Singida ni mipango ya Mungu,kwa hiyo kama kuna mtu nilikwaza katika utendaji wangu anisamehe nilikuwa natekeleza majukumu ya kazi," alisema.
Nao wenyeviti wa Halmashauri za Wilaya Mkoa wa Singida pamoja na wakuu wa wilaya walimpongeza Serukamba kwa utendaji wake uliotukuka ambao muda wote alikuwa vijijini kukagua miradi na kuhamasisha matumizi ya mbolea.
Негізгі бет VIONGOZI MKOANI SINGIDA WAELEZA KUGUSWA NA UTENDAJI KAZI WA SERUKAMBA
Пікірлер