WALIMU 300 WA SEKONDARI NCHINI KUPATIWA MAFUNZO YA TEHAMA
Tarehe 07 Oktoba 2024, Waziri wa Habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari, Mhe. Jerry William Silaa (Mb), amefungua mafunzo ya TEHAMA kwa walimu 300 wa shule za sekondari katika hafla iliyofanyika Taasisi ya Teknolojia Dar es Salaam (DIT) jijini Dar es Salaam.
Mafunzo hayo yanadhaminiwa na Serikali kupitia Mfuko wa Mawasiliano kwa Wote (UCSAF) na yanaendeshwa na vyuo vikuu vya DIT (Dar es Salaam), MUST (Mbeya), na UDOM (Dodoma), ambapo kila chuo kimepata washiriki 100.
Akizungumza wakati wa ufunguzi wa mafunzo hayo, Waziri Silaa amesema jambo hilo ni la kujivunia na linaonesha jitihada kubwa za Serikali chini ya uongozi imara wa Rais wa Jamhuri wa Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, katika kuhakikisha tunaziba pengo la kidijitali kwa kushirikisha walimu kutoka maeneo mbalimbali ya nchi, hususan shule za vijijini.
Waziri Silaa alisisitiza kuwa mafunzo haya ni hatua muhimu katika kuhakikisha walimu wanakuwa na uwezo wa kutumia vifaa vya TEHAMA kwa ufanisi zaidi. Aliongeza kuwa mafunzo haya si tu yatawasaidia katika matumizi ya vifaa vya TEHAMA, bali pia kuwajengea uwezo wa kufanya marekebisho madogo ya vifaa pindi vinapopatwa na hitilafu, pamoja na kuwasaidia kutumia programu mbalimbali za kidijitali ambazo ni muhimu katika ulimwengu wa sasa wa teknolojia.
Pia, Waziri Silaa alieleza kuwa Serikali kupitia UCSAF inaendelea na utekelezaji wa mradi mkubwa wa kufikisha huduma za mawasiliano vijijini, ambapo jumla ya minara 758 itajengwa katika kata 713 zenye vijiji 1,407. Pindi mradi huu ukikamilika, jumla ya wananchi milioni 8.5 watanufaika na huduma hiyo muhimu ya mawasiliano. Hadi sasa, jumla ya minara 279 kati ya 758 imewashwa, ikiwa ni sawa na asilimia 36 ya utekelezaji wa mradi wote.
Mhe. Silaa alitoa rai kwa watoa huduma wa mawasiliano kukamilisha utekelezaji wa mradi huu kwa sababu hatukusudii kuongeza muda wa ujenzi wa minara pindi muda wa mikataba utakapokwisha ifikapo tarehe 13 Mei 2025. Aliwataka wakandarasi wote waliopewa jukumu la kujenga minara hii kuhakikisha wanaifanya kazi hiyo kwa ufanisi mkubwa na kumaliza kabla ya muda wa mkataba kuisha.
Негізгі бет WALIMU 300 WA SEKONDARI NCHINI KUPATIWA MAFUNZO YA TEHAMA
Пікірлер