Rais wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli tarehe 19 Desemba, 2018 ameweka jiwe la msingi la upanuzi wa barabara ya Morogoro Jijini Dar es Salaam katika sehemu ya kuanzia Kimara hadi Kibaha yenye urefu wa Kilometa 19.2.
Akizungumza katika sherehe hizo Rais Magufuli amewapongeza wananchi wa Dar es Salaam kwa kupatiwa mradi huo mkubwa na kubainisha kuwa pamoja na barabara hiyo Serikali ya Awamu ya Tano inaendelea kuboresha miundombinu ya Dar es Salaam ambapo barabara zenye jumla ya kilometa 212 zinajengwa kwa gharama ya shilingi Bilioni 660.
Kuhusu fidia kwa nyumba zilizovunjwa wakati wa upanuzi wa barabara hiyo Rais Magufuli amewataka wanasiasa kuacha kuwapotosha wananchi kuwa watalipwa fidia, na amesema Serikali haitalipa fidia kwa mtu yeyote aliyejenga katika eneo la hifadhi ya barabara kwa mujibu wa sheria.
“Kuna wanasiasa wanataka waonekane wao ndio wanawatetea wananchi na wanasema Serikali itoe fidia, nataka niwaambie ndugu ukivamia barabara unatafuta umasikini, fidia haipo, fidia haipo, narudia fidia haipo” amesisitiza Rais Magufuli na kuwataka Watanzania kote nchini kuacha kuvamia maeneo ya hifadhi ya barabara na kujenga makazi.
Rais Magufuli ametoa wito kwa Watanzania kuendelea kulipa kodi na kwamba Serikali itaendelea kuhakikisha kodi inayokusanywa inasimamiwa vizuri kwa kuelekezwa katika miradi ya maendeleo ikiwemo ujenzi wa barabara, kuendeleza elimu, afya na kuboresha upatikanaji wa maji ukiwemo mkoa wa Dar es Salaam ambao kwa sasa unapata maji kwa asilimia 75.
Rais Magufuli amewaonya Madiwani wa Jiji la Dar es Salaam waliokuwa wakichelewesha kuanza kwa ujenzi wa kituo kikuu cha mabasi kutokana na kubishana juu ya mkandarasi wa kukijenga na kubainisha kuwa “Nilikuwa nawafuatilia jinsi mnavyobishana na leo mngekuwa bado mnabishana nilipanga nitangaze kuondoa fedha hizo (shilingi Bilioni 50) na kupeleka mahali pengine, ndugu zangu viongozi naomba tutangulize maslahi ya wananchi, sio maslahi yetu binafsi”.
Негізгі бет HOTUBA YA RAIS MAGUFULI ALIPOWEKA JIWE LA MSINGI UPANUZI WA BARABARA KIMARA - KIBAHA
Пікірлер: 2