MPANGO JUMUISHI WA WAHUDUMU WA AFYA NGAZI ZA JAMII KUANZA WILAYA YA TANGA NA HANDENI
Katika kuimarisha utoaji wa huduma za Afya msingi Nchini Serikali kupitia wizara ya Afya kwa kushirikiana na Ofisi ya Rais TAMISEMI na wadau mbalimbali ikiwemo Taasisi ya Benjamini Mkapa imeandaa mpango jumuishi wa huduma za afya kwenye ngazi za jamii.
Akizungumza Katika kikao cha utambulisho wa mpango jumuishi wa kitaifa wa wahudumu wa afya ngazi ya jamii katika mkoa wa Tanga, Mkuu wa Mkoa huo Mhe. Balozi Dkt Batilda Burian amesema mpango huo utaanza kwenye Halmashauri mbili za Wilaya ya Tanga Jiji na Handeni Mji ambapo watoa huduma 482 watafikiwa.
" Utekelezwa utafanyika kwa kipindi cha miaka minne kuanzia mwaka huu 2024/2025 hadi 2027/ 2028 ambapo wahudumu watachaguliwa kwenye ngazi za vitongoji na mitaa kwa Tanga jiji ni 362 na Handeni Mji watakuwa 120" alisema Balozi Dkt. Batilda.
Aidha Mkuu wa mkoa Dkt. Batilda ametoa wito kwa wananchi wa Mkoa wa Tanga kuchangamkia fursa hiyo kwa ajili ya kutoa huduma kwa jamii.
" Masuala ya utoaji huduma za afya ni wito kwa hiyo watakaopendekezwa wapatikane watu wenye wito na nia thabiti ya kutoa huduma kwa jamii" alisema Dkt Batilda.
Sambamba na hili Mkuu wa mkoa amewataka kuwaangalia na kuwapa nafasi watoa huduma ambao wanejitolea kwa kipindi kirefu katika utoaji huduma.
Kwa upande wake Afisa mradi kutoka Wizara ya Afya James Mhilu amesema Serikali imeamua Kuja na mpango huo lengo ni kuweza kufikia azma ya Afya kwa wote ifikapo mwaka 2030.
"Moja ya huduma muhimu katika kuboresha afya ngazi ya msingi ni kuboresha huduma ngazi ya jamii hivyo kama Serikali tunategemea kwa miaka mitano tutaajiri wahudumu zaidi ya 137,294 katika mikoa 26 ya Tanzania bara" alisema Mhilu.
Ili kufikia azma iliyokusudiwa mpango umezingatia vipaumbele mbalimbali ikiwemo masuala ya ustawi wa jamii na usafi wa mazingira.
Mwisho
Негізгі бет MPANGO JUMUISHI WA WAHUDUMU WA AFYA NGAZI ZA JAMII KUANZA WILAYA YA TANGA NA HANDENI
Пікірлер